Umuhimu wa kuwa na viota bora

Na Mkulima Mbunifu

Kuku anapotagia porini, mayai huliwa na wanyama kama vile nyoka na wengineo. Kuku pia anaweza kudhuriwa na wanyama hao na wakati mwingine kuibwa.

Kiota1

Viota ni mahali ambapo kuku hutaga mayai, kuhatamia na kuangua vifaranga. Hii inamaanisha kuwa viota ni sehemu muhimu sana ya kuzingatia ili kuweza kupata mayai mengi yaliyo salama pamoja na vifaranga.

Aina za viota

Kuna makundi mawili ya viota vinavyotumiwa na kuku pamoja na ndege wengine wafugwao.

• Kiota kilicho tengenezwa na kuku mwenyewe
Kiota2Hii ni aina ya viota ambavyo kuku huchagua mahali pa kutaga na kuhifadhi mayai. Inaweza kuwa mahali popote ambapo kuku ataona mayai hayataweza kudhurika au kuonekana. Kwa mfano, vichakani, stoo au kona yenye giza. Njia hii si nzuri kwani husababisha upotevu wa kuku na uharibifu wa mayai.

Kwa kutagia stoo au sehemu iliyojificha ya ndani, japokua ni sehemu salama ambayo haiwezi kufikiwa kirahisi na wezi au wanyama, mayai yanaweza kuharibika. Kuku akitaga sakafuni, sehemu yenye nailoni au magunia mayai yanaweza kuharibiwa na unyevu. Mayai hayo si mazuri kwa kutotoleshea. Itabidi mfugaji ayatumie au ayauze kwa ajili ya chakula.

Katika ufugaji wa ndani, kuku hutaga mayai sehemu yoyote hasa kipindi ambacho kuku huanza kutaga. Hii husababisha mfugaji kuyakanyaga mayai kwa bahati mbaya au kuku wenyewe kula mayai hayo na kupunguza uzalishaji wa mayai.

• Kiota kilicho andaliwa na mfugaji
Kiota3

Kuku wanapotengenezewe viota vizuri huhatamia kwa utulivu kuongeza uzalishaji
Hii ni aina ya viota vilivyo andaliwa kiustadi na kuwekwa mahali stahiki kwa kumrahisishia kuku sehemu ya kutagia. Viota hivi huwekwa ndani ya banda au sehemu nyingine iliyoandaliwa. Viota vya aina hii huandaliwa kwa kuzingatia idadi ya kuku wanaotarajiwa kutaga, pamoja na upatikanaji wa vifaa vya kutengeneza viota.

Mahitaji

Unaweza kutumia vifaa kama vile boksi la karatasi, mbao, nyasi, nguo aina ya pamba (isiwe ya tetroni), matofari na maranda. Boksi, tofali, na mbao husaidia kutengeneza umbo na ukubwa wa kiota. Nyasi maranda na nguo (viwe vikavu) husaidia katika uhifadhi wa mayai yasiharibiwe na unyevu, pia ni mazuri kipindi cha kuhatamia kwani hutunza joto.

Ukubwa wa kiota unatakiwa uwe ni wa kumwezesha kuku kuenea na kujigeuza. Hii ina maana kuwa unatakiwa uwe wastani wa sentimita 35 upana sentimita 35 na urefu sentimita 35.

Namna ya kupanga viota kwenye banda

Ili kuwa na ufanisi mzuri, inabidi idadi ya viota kwenye banda iwe robo tatu ya matetea yaliyofikia umri wa kutaga. Hii huondoa msongamano wa kutaga katika kiota kimoja. Kwa mfugaji mwenye kuku wengi inampasa kuchagua vifaa ambavyo atajengea viota vinavyoweza kutumia eneo dogo na huku akipata viota vingi.

Kwa kuku wanaohatamia, inabidi watengewe chumba chao ili kuzuia uchanganyaji wa mayai. Kila sehemu katika banda si nzuri kuweka viota. Hivyo, katika uchaguzi inakupasa uzingatie mambo yafuatayo:
• Viota visiwe karibu au chini ya kichanja cha kupumzikia, vyombo vya chakula na maji.
• Kiota kisiwe sehemu ambayo mfugaji atakua anapitapita. Mfano, karibu na mlango au dirisha.
• Kiota kisiwe mkabala na sehemu ambayo upepo mkali au mwanga utakua unaingia.

Wakati wa ujenzi wa banda unaweza kujenga vyumba viwili ambavyo kimoja kikubwa utatenga sehemu ya chakula, maji na sehemu ya kupumnzika.

Chumba cha pili utatengeneza viota tu ili kuku anayetaka kutaga aende huko. Kwa kufanya hivyo, kuku wachache watakua wakienda chumba hicho, na usumbufu kwa kuku wanaotaga utakuwa mdogo.
Kulingana na kiasi cha nafasi, unaweza kujenga viota mwisho wa banda na vyombo vya chakula na maji upande wa mbele karibu na mlango. Hii itasaidia kuku kushinda sehemu yenye chakula na maji hivyo kuepusha usumbufu kwenye viota.

Kuku wanaohatamia

Viota vya kuku wanaohatamia inabidi viwe sehemu tofauti na viota ambavyo kuku wanatagia mayai kila siku. Hii itasaidia kuzuia uchanganyaji wa mayai yaliyoanza kuhatamiwa na mapya. Viota hivyo viandaliwe vizuri kwani hukaa na mayai kwa muda mrefu. Ni vema kuwatenga kuku katika chumba chao ambapo watapatiwa maji na chakula.

Umuhimu wa viota
Kiota4

  • Kwa kuwa na viota vya kutosha itapunguza usumbufu wa kuingia kukusanya mayai kwa mfugaji.
    • Njia mojawapo ya kuzuia kuku kula mayai.
    • Upotevu wa kuku na mayai utapungua.
    • Utapata mayai bora kwa ajili ya kutotolesha.
    • Kupunguza mayai kupasuka, pia mayai kuwa safi.• Kuku kuwa huru wakati wa kutaga au kuhatamia.

 

Leave a Reply