Madhara ya mifuko ya plastiki kwa wanyama

Na Augustino Chengula

Mifuko ya plastiki imekuwa ikitumika kwa miaka mingi sasa hapa nchini kwa matumizi mbalimbali kubwa likiwa ni kubebea mizigo au bidhaa toka sokoni au mashambani. Mifuko hii imekuwa ikitumika mahala pengi duniani, tayari nchi kadhaa zimepiga marufuku matumizi ya mifuko ya plastiki kutokana na madhara yake. Mifuko hii ya plastiki ibuniwa kwa mara kwanza kabisa miaka ya 60 na Mhandishi kutoka Swideni ndugu Sten Gustaf Thulin. Tatizo kubwa la mifuko hii ya plastiki ni kutooza pale inapotupwa kwenye mazingira na kuifanya iendelee kukusanyika. Hivyo mifuko hii ikitupwa hovyo huzagaa kwenye mazingira na kluleta kero kubwa kwa jamii inayozunguka na viumbe wengine. Na matumizi yake makubwa ni kwa sababu mara nyingi mifuko hii hutumika mara moja tu toka sokoni kwenda nyumbani kisha hutupwa.

Madhara ya jumla ya mifuko ya plastiki

  1. Mifuko hii ikitupwa hovyo huchafua mazngira
  2. Mifuko hii inaweza kuchukuliwa na upepo kwenda kuharibu mazingira maeneo mengine yaliyo safi
  3. Mifuko hii inaweza kuchukuliwa na maji na kwenda kuziba mitaro ya maji na kusababisha mafuriko
  4. Mifuko hii inaweza kuchukuliwa na maji kwenda baharini na kuathiri viumbe wa maji
  5. Mbaya zaidi mifuko hii huliwa na wanyama wafugwao na wa porini na kuwasababishia vifo

Kwa mkitadha wa somo letu la leo, nitaelezea madhara ya mifuko ya plastiki kwa mifugo yetu.

 

Kwa nini mifugo hula mifuko ya plastiki?

Wanyama wengi hupenda kula mifuko hii ya plastiki kwa sababu mifuko hii hutumika kuwekea chumvi inayopendwa sana na wanyama wengi. Wakati mwingine wanyama hula mifuko ya plastiki kwa sababu ya njaa inayo wakabiri.

 

Hatari ya mifuko ya plastiki kwa wanyama

Mifuko ya plastiki inaweza kuliwa hasa na ng’ombe, mbuzi, kondoo na ndege. Mifuko au sehemu ya mifuko hii ikimezwa na wanyama hukwama kwenye matumbo yao na kuendelea kukusanyika taratibu humo tumboni. Madhara yake yanaweza kuwa:

  1. Kukosekana hewa- kwa wanyama wadogo kama mbuzi, kondoo au kuku na ndege wengine wanapotaka kula mifuko hii wanaweza kujiviringisha kichwani na kuwasabishia kukosa hewa taratibu. Msaada wa haraka ukikosekana huplekea kifo.
  2. Kunyonga- Pia hii inaweza kuwapata wanyama wadogo kama kuku, kondoo na mbuzi ambapo mifuko hii inaweza kujizungusha shindoni na kukaba shingo kunakoweza kupelekea kukosa hewa na kifo.
  3. Kumeza mifuko-Hii huwakumba wanyama wote ni huwa na madhara makubwa sana kwa mifugo. Mifuko hii ya plastiki ikimezwa huenda tumboni na kupunguza au kuziba njia ya chakula na kusababisha chakula kidogo kiruhusiwe kupita. Wakati mwingine hasa kwa wanyama wanaocheua ambao tatizo hili kwao limekuwa tishio, mifuko huenda kukaa kwenye tumbo la kuhifadhia chakula kabla ya kumeng’enywa kwa kuwa njia ya kuendelea huwa haiwezi kupita. Mifuko hii huendeleea kukusanyika taratibu tumboni. Wakati huo plastiki hujikusanya katika umbo la mviringo mithili ya mpira wa miguu.

 

Dalili za myama wenye mifuko ya plastiki

Kwa bahati mbaya ni vigumu kubaini myama mwenye mifuko ya plastiki, lakizi huambatana na dalili hizi

  1. Mnyama hupunguza kiasi cha kula
  2. Mnyama huanza kukonda na kuendelea hivyo hata baada ya kufanya matibabu kwa kutumia dawa
  3. Mwishowe mnyama mwenye mifuko ya plastiki hufa
  4. Ukimpasua ndani mnyama huyu utakutana na mifuko ya plastiki ikiwa imejivingisha vizuri kana kwamba kazi hiyo imefanywa na mtaalamu wa kutengeza mipira ya kuchezea watoto
Picha ya upande wa kushoto ni mbuzi wakila mifuko ya plastiki nay a kulia ni ng’ombe alikufa kwa kula mifuko ya plastiki na pembeni yake ni mifuko iliyokuwa ndani yake

Nini cha kufanya kuzia tatizo hili?

  1. Kupiga marufku matumizi ya mifuko ya plastiki- Kuna nchi kadhaa zimefanikiwa kwa kuja na mifuko mbadala kwa matumizi yanayofanana na mifuko ya plastiki mfano majirani zetu Kenya lakini pia upande wa pili wan chi yetu kule Zanzibar.
  2. Kuirusha mifuko iliyotumika viwandani ili wakaitengeneza upya- Hii itatengeza ajira na watu watakuwa hawatupi hovyo bali wataiuza au ikitupwa hovyo itaokotwa kwa ajili ya kuiuza
  3. Kuepuka kutupa mifuko hoovyo kwa kutupa maeneo maalumu na kuichoma au kuzika chini sana
  4. Kuwapatia mifugo madini ya kuramba au kwenye chakula ili kupunguza hamu ya kula mifuko ya plastiki.

 

UWE WA KWANZA KUEPUKA KUTUPA MIFUKO YA PLASTIKI HOVYO KUEPUSHA VIFO VYA MIFUGO

 

 

 

 

Leave a Reply