SEHEMU YA KWANZA SOMA HAPA
- KANUNI ZA KUFUATA UPANDE WA BIOSECURITY YA KUKU KILA SIKU
- a) Nyaraka na Mafunzo kwa wafanyakazi
- i) Kila shamba la kuku/hatchery iwe na nyaraka (document) ya Taifa inayohusu Biosecurity. (Sijui kama Tanzania tuna nyaraka hiyo).
Unaweza pia kuandaa nyaraka yako ya Biosecurity, kulingana na mazingira na ufugaji ulionao.
- ii) Kila mfanyakazi anatakiwa kupewa nakala ya nyaraka ya Biosecurity.
iii) Wafanyakazi wapewe mafunzo kuhusu Biosecurity na waelezwe umuhimu wa kuhakikisha inafanyika kila siku.
- b) Mabanda
- i) Eneo la kujenga mabanda.
– Chagua eneo lililo mbali na mashamba mengine ya kuku, ili kuzuia usambaaji wa magonjwa kutoka shamba moja kwenda jingine. Umbali kati ya mashamba, uwe angalau mita 500.
– Angalia upande upepo unapotokea. Banda la vifaranga yawe mwanzo, mabanda ya kuku wakubwa yafuate, ili upepo uanze kwenye banda la vifaranga kuelekea kwa wakubwa, na isiwe kinyume. Hii inasaidia vumbi au magonjwa ya kwenye kuku wakubwa yasihamie kwenye vifaranga.
– Epuka kujenga banda bondeni au karibu na njia za maji, ambapo panaweza kuwa na mafuriko na unyevunyevu muda mwingi.
– Usijenge maeneo wanayopita ndege pori wanaohama kutoka eneo moja kwenda jingine, kwani wanaweza kuhamisha vimelea vya magonjwa kutoka eneo moja kwenda jingine.
– Jenga banda angalau mita 300 kutoka kwenye barabara kubwa ya magari, kwani barabara hizo hutumika kusafirisha kuku wa kutoka mashamba mbalimbali.
– Mabanda ya kuku yasijengwe karibu na hatchery au mashine ya kusaga chakula cha kuku au sehemu maalum ya kuchinja kuku, kunyoyoa na kuwapack. Kutofautisha sehemu hizo ni njia kubwa ya kuzuia magonjwa kusambaa.
- ii) Ujenzi wa mabanda.
– Mabanda ya kuku wa umri tofauti, yajengwe mbali kutoka banda moja kwenda jingine. Umbali huo uwe angalau mita 30 kutoka banda moja hadi jingine.
– Eneo la mabanda liwekewe uzio (fence), ili kuzuia watu wasioruhusiwa kuingia. Pia kuzuia wanyama kama paka, mbwa, kuku wanaofugwa huria kuingia. Sehemu ya kuingilia watu na magari iwekwe na kutumika dawa ya kuua wadudu kama V-RID.
– Eneo la kuzunguka banda liwe safi muda wote. Eneo hilo likiwekwa sakafu ni vizuri zaidi, kwani itakuwa rahisi kufanyiwa usafi.
– Sehemu za banda zilizowazi ziwekwe waya (Chicken wire), ili kuzuia wadudu na wanyama kama paka, mbwa, panya vicheche, wasiingie bandani.
– Watu wote wanaoingia bandani, watumie njia sahihi ya lazima ya kuzuia magonjwa kuingia bandani. Mfano, kubadilisha viatu na kuvaa viatu maalum vya kuingilia bandani, kuvaa koti maalum la kuingilia bandani, kufunika nywele au kuvaa kofia maalum. Vitu hivyo visafishwe mara kwa mara na kutunzwa kwenye hali ya usafi. Kwenye mashamba makubwa ya kuku kuna eneo maalum la kuoga kwa kila anayeingia mabandani. Wafanyakazi wafundishwe namna ya kutumia eneo hili kwa usahihi.
– Sakafu ya banda iwe na mwinuko kidogo, ili maji ya mvua au maji ya kuoshea banda yasituame, na yaelekee nje ya banda.
– Eneo la kutunzia chakula lijengwe vizuri, kusiwe na unyevunyevu na joto kali ili chakula kisiharibike.
- c) Hatchery
– Hatchery ijengwe eneo lisilotuamisha maji.
– Nyumba ya hatchery iwe rahisi kufanyiwa usafi.
– Kwenye mlango wa kuingia hatchery kuwe na bango lenye maneno ‘Wanaingia Wahusika tu’
– Nyumba ya hatchery iwe na vyumba tofauti vya kubadilisha nguo wafanyakazi, kupokelea na kutunzia mayai ya kutotolesha, kutotolea (incubation), kuchambua vifaranga, kuchanja vifaranga na kuwapack kwenye mabox, kuosha vifaa na pa kutupia takataka.
– Mayai viza yaondolewe kwenye hatchery, mara tu yanapoonekana, na yachimbiwe eneo la mbali na hatchery.
– Vifaa vinavyotumika, meza, viti vya hatchery, visafishwe mara kwa mara kwa dawa ya kuulia wadudu kama V-RID.
– Wafanyakazi wa hatchery, waoshe mikono mara kwa mara kwa sabuni, hasa wanaposhika vifaranga na mayai ya kutotolesha.
– Vifaranga vitunzwe kwenye mabox safi.
- d) Kuku Wazazi
– Viota viwe safi muda wote. Kama viota vinawekewa matandazo (maranda, majani makavu au mchanga), hakikisha vinabadilishwa mara kwa mara.
– Mayai ya kutotolesha akusanywe/yaokotwe mara kwa mara kila siku, na yawekwe kwenye trays mpya au zilizosafishwa kwa dawa ya V-RID.
– Mayai machafu, yenye nyufa, yaliyovunjika na yanayovuja, yawekwe tofauti na mayai mazuri, na yasitumike kwenye kutotolesha.
– Mayai ya kutotolesha yasafishwe/yaondolewe uchafu mara tu yanapokusanywa bandani.
– Mayai ya kutotolesha au trays ziandikwe tarehe ya kutagwa, ili iwe rahisi kujua muda wa mayai tangu kutagwa.
– Mayai ya kutotolesha yatunzwe kwenye Chumba maalum kisafi. Chumba hiki kisafishwe mara kwa mara ili kuzuia bacteria wasiingie kwenye mayai na kuyaua.
– Kuku Wazazi waendelee kupewa chanjo ya Newcastle, kila baada ya wiki 10, kwa maisha yao yote.
– Magari, baisikeli, pikipiki zinazokuja shambani kuchukua kuku, yapuliziwe dawa ya kuulia wadudu, kabla ya kuingia eneo la shamba.
– Wabebaji wa kuku kutoka nje, nao wapuliziwe dawa kabla ya kuingia bandani.
– Vifaa vinavyotumika kubebea kuku, kama cage, matenga ya miti au plastic, yasafishwe kwa dawa ya kuulia wadudu, kabla ya kuingia bandani.
– Baada ya kuku kuchukuliwa, milango ya banda ifungwe, isipokuwa muda wa kutoa matandazo na kusafisha banda. Baada ya kusafisha banda, milango ifungwe tena.
– Matandazo na mbolea zisiachwe kwenye banda kwa muda mrefu baada ya kutoa kuku. Pia visitolewe bandani na kuwekwa nje ya banda. Vipelekwe eneo maalum la mbali na mabanda, au vipelekwe shambani.
- f) Wafanyakazi
- Wafanyakazi wazalishaji.
– Wafanyakazi wanaohusika na shughuli za uzalishaji za shamba na wanaishi eneo la shamba, wasiende kwenye mashamba mengine ya kuku bila sababu maalum.
Wakienda huko, wanaporudi, waoge mwili mzima na wabadilishe nguo, wavae nguo safi.
– Wafanyakazi wavae nguo safi zilizopigwa pasi kila siku asubuhi.
– Kuwe na dawa ya kuulia wadudu kama V-RID muda wote, ili wafanyakazi wanawe mara kwa mara kwa dawa hiyo, huzuia maambukizi ya vimelea vya magonjwa
– Wafanyakazi wa kike wenye nywele ndefu ambazo hazioshwi kila siku, wavae vitambaa au kofia kichwani.
- Wageni, majirani na marafiki.
– Kuwe na mavazi maalum kama koti na viatu vya kuingia nayo shambani. Wageni wavae mavazi hayo kabla ya kuingia shambani. Mavazi hayo yafuliwe mara tu baada ya kutumika.
– Wageni wanawe mikono kwa kutumia V-RID. Pia wasishike kitu chochote bila kuruhusiwa.
iii. Mafundi Ujenzi, umeme, maji.
– Mafundi wanaofuga kuku majumbani kwao, wanapokuja shambani, waoge mwili mzima na wabadilishe nguo na viatu na wavae kitu cha kufunika nywele.
– Vifaa vitakavyotumika shambani, visafishwe kabla ya kuingia shambani, ili kuzuia vumbi kuingia shambani.
– Magari yote yapakiwe nje ya shamba, isipokuwa kama kuna ulazima wa gari kuingia, lipulizwe dawa ya kuulia wadudu kabla ya kuingia shambani.
- g) Uendeshaji.
- Maji.
– Hakikisha maji yanayotumika kwa mifugo ni safi na salama.
– Kama unatumia maji ya kisima, tafuta wataalamu wayapime na kuona kama yanafaa kwa mifugo.
– Chakula kinachomwagika kikusanywe mara moja, na eneo kilipomwagika pasafishwe. Chakula kinachomwagika kinawavutia ndege na panya.
– Majani yaliyopo kwenye eneo la shamba yakatwe mara kwa mara, ili kuzuia panya na vicheche wasijifiche humo. Pia kuzuia mazalia ya wadudu.
– Sehemu za kuwekea dawa mlangoni mwa banda, ziangaliwe kila siku na kuhakikisha maji yenye dawa yapo muda wote, na ni safi.
– Mbolea zitolewe mara kwa mara bandani, na zikawekwe mbali na mabanda au shambani.
– Maji yasituame eneo la banda.
- h) Utunzaji kumbukumbu.
– Weka kumbukumbu za vifo vya vifaranga na kuku wakubwa na uchunguze sababu za vifo hivyo.
– Weka kumbukumbu ya chanjo na dawa unazowapa kuku, pia na duka unaponunulia, ili kukiwa na tatizo la chanjo au dawa iwe rahisi kujua duka linalohusika.
- i) Unapouza kundi la kuku.
– Maelezo ni kama ya (e) hapo juu.
MAKALA HAYA YAMEANDALIWA NA:
Aquinus Farms Limited
0655347932